Wadau Sekta ya elimu wametakiwa kuendeleza ushiriki wao kuimarisha miundombinu Kwenye Sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na ujenzi wa madarasa, karakana na nyenzo za kijifunzia ili kuwa na mazingira bora ya kufundishia na kujifunza
Hayo yamezungumzwa na Katibu Mkuu Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia Profesa Carolyne Nombo jijini Dodoma wakati akifungua mkutano wa pamoja wa Tathimini ya Maendeleo ya Sekta ya Elimu ambapo amesema katika kutekeleza sera na mitaala iliyoboreshwa ni vyema kuwepo kwa Mafunzo endelevu kazini kwa walimu Ili kuwa Mtanzania aliyeelimika na mwenye ujuzi ataochangia maendeleo endelevu katika Nchi na Dunia kwa ujumla.
Profesa Nombo ambaye alimwakilisha Waziri wa Wizara hiyo Profesa Adolf Mkenda alisema, Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia ,tayari imekamilisha Mpango wa Maendeleo wa Sekta ya Elimu na kwamba inaendelea na uandaanji wa miongozo mbalimbali itakayosaidia katika utekelezaji wa sera na mitaala iliyoboreshwa.
Alisema,lengo la kufanya hivyo ni kuongeza ubora na ufanisi katika sekta ya elimu na kuleta matokeo chanya kwa wananchi na Taifa kwa ujumla .
Profesa Nombo alitumia nafasi hiyo kuwaasa Wadau wa sekta ya Elimu kuendeleza ushiriki wao kuimarisha miundombinu kwenye sekta ya elimu ikiwa ni pamoja na ujenzi wa madarasa, karakana na nyenzo za kujivunzia Ili kuwa na mazingira bora ya kufundishia na kujifunza.
“Uwepo wa utoshelevu wa miundombinu na vifaa vya kujifunzia na kufundishia utasaidia kukidhi ongezeko la wanafunzi katika ngazi mbalimbali za elimu na hivyo kuwa na mazingira bora kwa wao kujifunza.”alisema Profesa Nombo
Alisema hatua hiyo inalenga katika kutumiza ndoto ya nchi ya kuwa na mtanzania aliyeelimika, mwenye ujuzi na mtazamo chanya atakaochangia maendeleo endelevu katika nchi na dunia kwa ujumla
Hata hivyo alisema ,pamoja na mafanikio makubwa katika sekta ya Elimu , bado kuna uhitaji wa kuhakikisha ubora wa elimu, utoshelevu wa walimu, wakufunzi na wahadhili hususan wa sayansi, hisabati ,teknolojia na amali.
Awali, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Elimu, Sayansi na Tekinolojia, Dkt. Charles Mahera alitaja baadhi ya mafanikio makubwa katika sekta ya Elimu kuwa ni pamoja na kupanua upatikanaji wa elimu, kuimarisha ubora wa elimu kupitia mafunzo kwa walimu, kuimarisha upatikanaji wa nyezo za kufundishia, maboresho ya sera na mitaala na kuimalisha ubunifu na tekinolojia.
Alisema kikao hicho kitakuwa ni fursa kwa serikali na wadau wa elimu kuja na mikakati itakayosaidia kuendelea kuboresha sekta ya elimu.