Makamu Mkuu wa Taasisi ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) Taalamu, Utafiti na Ushauri wa Kitaalam Prof. Ezekiel Amri ameipongeza timu ya wadau walioshiriki katika warsha ya kuboresha mitaala mipya katika fani za Uhandisi Umeme na Nishati Jadidifu katika ngazi ya Uzamili na Stashahada.
Ameyasema hayo leo tarehe 4/6/2024 kwenye Warsha ya siku moja iliyofanyika kwenye Maabara ya Festo iliyopo Kampasi Kuu ya Taasisi hiyo jijini Dar es salaam.
Prof.Amri ameeleza lengo la kuwaalika wadau ni kupokea maoni yatakayowezesh kuandaa mitaala ya programu hizi mbili zilizopendekezwa ili kuweza kutoa mitaala itakayokidhi mahitaji ya soko la ajira.
” Leo tunaprogramu mbili za kupokea maoni ili tuweze kuandaa mitaala inayoendana na soko la ajira. Maoni mtakayotoa yatawezesha kuziboresha zaidi ili tuweze kutoa mafunzo yanayoendana sambamba na kile kinachofanyika viwandani kwa kufanya hivyo tutakuwa tumetoa suluhu ya mahitaji yaliyopo kwenye jamii lakini kumuwezesha mhitimu kuajirika au kujiajiri hivyo kwa mchanganyiko wenu huu naamini kabisa maoni yenu na mawazo yenu yatazalisha programu zitakazokidhi mahitaji hayo” amesema Prof. Amri
Kwa upande wake mratibu wa Mitaala wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT),Dkt.Dalton Kisanga ameeleza kuwa taasisi imeandaa warsha hii kwa ajili ya kuboresha mitaala kutokana na mabadiliko makubwa viwandani na hususani mabadiliko ya teknolojia na hayo ndiyo yanauotulazimu kuboresha mitaala ili Taasisi iweze kuzalisha watu wenye ujuzi sawa sawa na kile kinachofanyika viwandani.
“Huu ni utaratibu wa kuboresha mitaala kwa kuwa teknolojia inabadilika na mahitaji ya soko nayo yanaongezeka kila mara hivyo Taasisi sasa imewaita wadau kutoka maeneo tofauti tofauti hapa tuna wadau kutoka viwandani,mamlaka zinazotusimamia,tuna waajiri na wanafunzi lengo letu ni ili kupata mawazo yao ili tuweze kutoka maboresho yatakayotusaidia.”amesema Dkt.Kisanga.