Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Kanda ya Mtwara, ni moja ya wadau walioshiriki kwenye siku ya Sheria nchini ambayo kimkoa imeadhimishwa katika viwanja vya Mahakama kuu Mtwara leo Tarehe 03 Februari 2025.
Maadhimisho hayo yameongozwa na Mhe. Jaji Mfawidhi Kanda ya Mahakama kuu Mtwara Rose Edward Ibrahim, na kuhudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Abdallah Mwaipaya aliyemuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Kanali Patrick Sawala.
Wakili wa Serikali Mkoa, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Nunu T. Mangu ameeleza kuwa ni jukumu la ofisi hiyo kuhakikisha kuwa inatoa ushauri wa kisheria ambao utasaidia Serikali na Taasisi zinazosimamia haki kutunga sheria zenye maslahi kwa Serikali na Taifa kwa ujumla.
Akitoa salamu zake kwa washiriki mbalimbali waliojitokeza kwenye viwanja hivyo, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Abdallah Mwaipaya ameielezea siku ya sheria kuwa ni siku muhimu.
Ameeleza kuwa Mahakama ni muhimuli muhimu wa dola unaohakikisha kuwa haki inapatikana kwa wakati, usawa na wajibu mkubwa.
Kwa upande wake Mhe. Jaji Mfawidhi Kanda ya Mahakama kuu Mtwara Rose Edward Ibrahim, amesema mahaka imeendelea kuboresha utendaji kazi wake kwa wananchi, huku changamoto mbalimbali zikiendelea kutatuliwa.
“Tunatambua kuwa zimekuwepo changamoto mbalimbali zinazozikabila mahakama, lakini zimeendelea kutatuliwa ikiwa ni pamoja na uimarishaji wa miundombinu ambayo sasa tunaweza kufanya kazi kwa njia ya mtandao” ameeleza Mhe.Jaji Mfawidhi Rose Ibrahim.