KONA YA FYATU MFYATUZI: Kupinga uraia pacha tunajifyatua wenyewe

Juzi, nilipata mstuko, mshangao na masikitiko sina mfano. Nilisoma taarifa kuwa Kenya inafyatua takribani dolari bilioni tano toka kwa diaspora dhidi ya dolari bilioni 1.50 za uwekezaji. Kwa taarifa hii, Kenya inafyatua njuluku ndefu kuliko misaada na uwekezaji/uchukuaji.

Niligundua ni kwa nini kaya yenye mafyatu wachache na ardhi kidogo isiyofikia hata nusu ya mafyatu wetu na neema asilia kiduchu ikilinganishwa nasi inakuwa na uchumi mkubwa kuliko sisi. Katika kutafakari na kufikiri, niligundua kuwa tunajifyatulisha na kufyatuliwa kutokana na ukale, woga na mtima nyongo.

Sambamba na Kenya, siku chache kabla ya kutolewa taarifa hii, sirkal iliangaza mikakati ya kupata njuluku za diaspora wetu bila kustahiki wala kujenga mazingira mazuri. Kwani, inakataa uraia pacha huku ikishobokea wawekezaji ambao wengi ni wachukuaji tu.

Jikumbushe tulivyofyatuliwa na matapeli kutoka India waliojifanya kuwekeza kwenye Shirika la Reli, wakaishia kutufyatua njuluku hata mabehewa. Kabla ya hapo, walikuja ABSA wakafyatua banki yetu ya Biashara na kusepa. Walifuatia BAE Systems, Barriki dhahabu, Chavda, EPA, ESCREW, IpTelo, Mabilioni ya Njaa Kaya, Meremetuka, na nyingine nyingi ambapo tulipigwa njuluku ndefu tu. Kama haitoshi, jikumbushe Richmonduli-Dowan, Kagoda, mwanakaya gold na mazabe mengine yaliyofyatua na kufilisi kaya yetu. Tatizo ni nini?

Wakati wachukuaji wanakuja kufyatua njuluku iliyokwisha tengenezwa, tunakosa njuluku wanayotengeneza wanadiaspora wetu. Akili au matope? Tunazidiwa na vijinchi kama Gambia chenye watu milioni 2.4 na ukubwa wa kilomita za mraba 11,300 kinachozidiwa na mkoa mdogo kama Kilimanjaro wenye ukubwa wa kilomita za mraba 13,250 kilichoingiza dolari 775.6 ikilinganishwa na Bongolalaland iliyoingiza dolari 570, huku uwekezaji ukiwa wa thamani ya dolari milioni 931.60. Fedha ya diaspora haina masharti na shaka kama uwekezaji uliogeuka upigaji.

Tunahitaji uongozi unaojiamini, wenye ubunifu, wa kisasa, na usiotaka kuvuna usipopanda kama ilivyo. Unataka wabongo wa diaspora watume njuluku wakati huwatambui wala kuwamotisha? Inaingia akilini kweli? Hata unapotaka kuwafyatua kuwapa hadhi maalumu, unawazingua na kuvuta miguu.

Ajabu, uraia huu huu unaoonekana mali wakati si mali kitu wanajizolea hata wacheza kandanda! Tunamkomoa na kumfyatua nani? Wawekezaji wanakuja na kujizolea njuluku kwenye shamba la bibi hadi mapipa yetu yanakamatwa ughaibuni na kushitakiwa na kufyatuliwa mamilioni ya dolari. Rejea mamilioni ambayo yeshalipwa au yatalipwa kutokana na uzwazwa na woga wa kimfumo.

Mfano, mnataka wanadiaspora walete njuluku home wakati hawana haki za kumiliki mali? Mnawapa hadhi maalumu. Nani aliwapa mamlaka haya wakati Sir God aliwaumbia Bongo? Tunamkomoa na kumfyatua nani zaidi ya kujikwamisha, kujikomoa na kujifyatulisha? Ukiangalia sababu kubwa ya kuogopa uraia pacha si nyingine zaidi ya woga wa siasa za majitaka. Kwani, hizo kaya zilizotoa uraia pacha zimepungukiwa nini? Je, mafisi na mafisadi wote wana uraia pacha?

 Rafiki yangu Profesa Mutua, mwenye uraia wa Kenya na Marekani aliwahi kugombea ujaji mkuu akanyimwa kutokana na kuwa mwanafunzi wa jaji mkuu aliyekuwa anamaliza muda wake. Hapakuwa na tatizo na uraia. Ukiachia huyo, Baba wa taifa la Senegal, Leopord Sedar Senghor alikuwa na uraia pacha na bado alikuwa rais aliyeleta uhuru na kufanya mambo makubwa kwa Afrika.

Inakuwaje sirkal yenye kuogopa na kukataa uraia pacha inaendeshwa na njuluku toka majuu mbali na chaguzi zake kugharimiwa na fedha hiyohiyo? Kunani hapa? Tuambiane ukweli bila kuogopana.

Kuna kipindi nilimsikia fyatu mmoja mnene, mwoga na zwazwa akisema eti tukiruhusu uraia pacha, wageni watachukua ardhi yetu. Ajabu! Mbona wageni wengi walikwishakujitwalia ardhi? Hiyo ardhi tunaifanyia nini zaidi ya kuitelekeza tukitegemea kuagiza majanki toka nje? Nani anaweza kuamini kuwa kaya yenye uwezo wa kuzalisha mchele hata kulisha eneo zima la Afrika Mashariki ingeagiza mchele wenye thamani ya dolari 27.49 milioni toka Thailand mwaka 2023? Yaani tunalishwa na nchi yenye ukubwa takriban nusu yetu ikiwa na kilomita za mraba 513,120 na idadi ya watu 64,785,90? Tukifyatuka na kusema tumerogwa, mtasema tunatukana kweli?

Miaka michache iliyopita, bi mkubwa wangu alikwenda uhamiaji kutafuta passport yake na za wanetu wakati akijiandaa kuja huku. Aliulizwa maswali ya kipuuzi mfano, unakwenda kule kufanya nini? Unamuulizaje fyatu mzima tena mjanja anakwenda majuu kufanya nini? Wewe inakuhusu nini? Mbona mnapotaka tulete njuluku home hamuulizi kaipataje?

Juzi nilikuwa napitia tovuti ya sirkal inayosuasua juu ya vibali vya kusafiria nje. Hapa Kanada hakuna kitu kama hicho. Kwa nini kumsumbua mtu akwambie anakwenda kufanya nini ughaibuni utadhani taahira? Wapo wanaosema eti wanafanya hivyo kuepuka mafyatu kwenda kufanya uhalifu huko. Kwani hakuna sheria? Je, hawa wanaopewa hawafanyi uhalifu, hasa uuzaji bwimbwi?

Kama fyatu anataka kwenda ughaibuni, mpe pasi asepe. Mengine atajijua. Kwanza, hata balozi zetu ughaibuni hazina mpango wala utaratibu wa kuwasaidia wabongo walioko nje, vinginevyo iwe ni kwenye kuunga juhudi na mambo mengine ya siasa za majitaka.

Tufikie mahali tukue na kukomaa na kuacha uzamani na woga. Vinatuchelewesha na kutufyatua na kutufyatulisha. Hivi samaki ana miguu mingapi?

Related Posts