Wenye ulemavu kukutana kujadili changamoto, fursa Kilimanjaro

Moshi. Wakati watu wenye ulemavu wakikumbana na changamoto za unyanyapaa katika baadhi ya familia, jamii imetakiwa kuwathamini, kuwasikiliza, na kutowafanya wapweke, bali kuwaonyesha upendo kama ilivyo kwa watu wengine.

Kutokana na hali hiyo, Mkoa wa Kilimanjaro kupitia shirika lisilokuwa la kiserikali la New Life Foundation, litawakutanisha wenye ulemavu kutoka maeneo mbalimbali ya mkoa huo Februari 7, 2025 ili kuwaweka pamoja kwa lengo la kusikiliza changamoto zinazowakabili.

Pamoja na kusikiliza changamoto hizo, wameandaliwa tamasha maalumu la ‘The Night to Shine’, ambapo wanaume watavaa mavazi ya kifalme na wanawake watavalishwa mavazi ya kimalkia.

Lengo la tamasha hili ni kuwawezesha wenye ulemavu, ambao mara nyingi hawawezi kufunga ndoa, kuwa na nafasi ya kujitokeza na kusherehekea siku hiyo kivyao.

Akizungumzia tamasha hilo, Mkurugenzi wa Shirika linalojihusisha na masuala ya watoto la New Life Foundation, Mchungaji Glorious Shoo amesema jamii inatambua kuwa wenye ulemavu wanayo haki ya kupendwa na kuthaminiwa kama walivyo watu wengine.

 “Kutakuwa na usiku maalum wa ‘The Night to Shine’ kwa ajili ya kuwatambua na kuwathamini wenye ulemavu katika jamii zetu. Tutasikiliza changamoto zao, lakini pia tutafurahi pamoja nao na kuifanya siku hiyo kuwa maalumu kwao,” amesema mchungaji Shoo.

Ameongeza kusema kuwa binadamu wote ni sawa na kwamba, bila kujali umbile, kabila, au dini, kila mtu anayo haki sawa na mwenzake.

Hivyo, wenye ulemavu nao wanahitaji kupendwa na kuthaminiwa kama walivyo watu wengine.

“Tunawahimiza Watanzania tushirikiane kwa pamoja. Hii isizuiliwe tu hapa Kilimanjaro, bali iwe na mikoa mingine. Tuwaonyeshe upendo ndugu zetu waliopata matatizo ya ulemavu.

Hivyo, jamii tuna wajibu wa kuonyesha kwamba tunawajali,” amesema Shoo.

Naye, Mratibu wa tamasha hilo, Gerald Simon, amesema kuwa Februari 7, mwaka huu wanatarajia kuwakutanisha watu wenye ulemavu 41 kutoka maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Kilimanjaro.

“Siku hii itakuwa maalumu kwa hawa ndugu zetu. Lengo letu ni kuwaambia kwamba tunawathamini na kuwaonyesha upendo,” amesema Simon.

Related Posts