NCAA, kupeleka Wanawake 800 kutalii Ngorongoro, kuunga juhudi za Rais samia kutangaza utalii

Na Seif Mangwangi,Arusha

ZAIDI ya wanawake 800 wanatarajia kutembelea Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), ikiwa ni katika kuelekea kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya Wanawake Duniani, 8 Machi 2025, ambapo Kitaifa itafanyika Jijini Arusha.

Imeelezwa kuwa lengo la kutembelea hifadhi hiyo mbali ya kujionea vivutio vingi vilivyoko katika hifadhi hiyo pia ni kujionea kazi kubwa iliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan kutangaza utalii kupitia filamu za Royal Tour na Amazing Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 22, 2025 Kamishna msaidizi wa Uhifadhi katika Mamlaka hiyo, Mariam Kobelo amesema safari hiyo itafanyika februari7, 2025 siku moja kuelekea kwenye kilele cha siku ya kitaifa itakayofanyika Jijini Arusha.

Amesema kwa kushirikiana na kampuni ya utalii ya Tanzanite Cooperate, bodi ya utalii pamoja na ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha wanawake watakaopata nafasi ya kusafiri kwensa hifadhini watachangia kiasi cha shilingi 170,000 ambapo fedha hiyo itatumika kulipia huduma zote muhimu.

” Wanawake wa Ngorongoro tumepanga kuwapeleka wanawake wa Tanzania kutalii na kuona mambo makubwa ambayo Rais Samia ameyafanya kupitia filamu ya Royal Tour na Amazing Tanzania, watalipia kiasi kidogo cha 170,000 ambapo utapata chai ya asubuhi chakula cha mchana, kiingilio na gharama ya usafiri” amesema Mariam.

Amesema pia kwa kushirikiana na jeshi la polisi kitengo cha trafiki ulinzi umeimarishwa kuhakikisha kila mtu atakayesafiri anakuwa salama bila kupata tatizo lolote awapo safarini.

Aidha Kamishna wa uhifadhi Mariam amesema pia wanawake katika hifadhi gya Ngorongoro wamepanga kufanya usafi kwenye barabara ambazo watalii hupita kuingia katika hifadhi hiyo pamoja na kwenda hospitali kutoa misaada kwa wagonjwa.

Mkurugenzi wa kampuni ya kitalii ya Tanzanite cooperate, Eline Mwangomo amesema safari hiyo ya siku moja itaanza saa 12 asubuhi katika ofisi za Mkuu wa Mkoa kuelekea Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro na kurejea jioni Arusha.

 

Related Posts