KONA YA FYATU MFYATUZI: No reforms, no elections ilhali tushageuzwa, kuchakachuliwa!

Mjini kuna stori ya no reforms no elections, kwa Kisambaa, hakuna mageuzi, hakuna uchaguzi. Kwanza, sijui kama mafyatu waliofyatuliwa na shida wanaweza kufyatuka wakawafyatua wawafyatuao.

Wapo wanaosema eti mafyatu watinge mitaani na kukinukisha! Loo! Mbona mwaota mchana!

Mnategemea mafyatu waliofyatuliwa wakafyata wafyatuke watekwe na kupotezwa? Nani afyatuke afyatuliwe shaba kama Tunda Lishe?

Waliokwishatekwa, kuteswa na kupotezwa watoshe. Nasikia ngebe za mageuzi kutaka uchaguzi huru na wa haki.

Nani kawaambia duniani kuna haki au uhuru hasa kwa mafyatu wafyatuliwa? Hamjaambiwa kuwa haki hupokwa na iko peponi au motoni? Acheni ufyatu.

Mkikomaa, nateka na kupoteza mkapate haki huko mtakakoharakishiwa. Siwatishi au kufyatuka kifyatu. Wangapi weshatekwa na kupotezwa? Nini kimefanyika?

Mnataka kumfyatua nani? Uchaguzi ni dhana tata. Unaweza kuchagua hata kuchakachua ukajiaminisha umechagua.

Waweza kutochagua ukapitisha bila kupingwa ukajiridhisha umechagua japo hukuchagua. Mnataka mageuzi. Nani anataka kugeuzwa kama pweza kikaangoni ilhali walaji weshajiandaa kumfyatua hata bila kumpika au kumgeuza?

Kubalini yaishe. Baada ya wenye kaya kufyatua na kupitisha ‘mpendeka na mkubalika’ bila kupingwa hata walipotaka kumpinga, wapingaji wamefyatuka.

Wanataka wamfyatue kupitia mageuzi. Wanafyatuka eti watasusa uchakachuaji. Ebo! Mkisusa, wachakachuaji watachakachua, kufyatua, na kula. Mmesahau mazoea au mwajitoa akili? Mnakuwa kama hamjui inshu mafyatu wangu!

Mafyatu wangu mlofyatuka na kutaka kufyatua, mnataka kujifanya hamjui manufaa ya kupitisha bila kupingwa kwa kaya na mafyatu waliofyatuliwa wakagoma kufyatuka na kufyatua!? Nazoza na mafyatu mliofyatuka mkatishia kususa uchakachuaji. Nyie mafyatu msiofyatuka hadi mkafyatuliwa nani aliwaroga kudhani kuwa mageuzi yanaweza kuleta mageuzi ilhali gegezi?

Mkitaka mageuzi, jigeuzeni mfyatuke muache kufyatuliwa. Haki haiombwi, hupokwa. Hivyo, kususa ni kusuasua na kufyatuliwa. Badala ya kusema no reforms no election mseme we must fyatuka and fyatua them to grab our rights. Period. Tukubaliane hata kwa kupingana. Mnapingaje mteule wa Mungu mwenye maono na ndoto visivyo vya kifyatu? Hamjui kuwa wateule wa Mungu hupaswa kutawala milele kama Ngwazi wa kwa akina Bwinobwino? Hamuoni maajabu yalotendwa kama ‘kufungua’ kaya iliyokuwa imefungwa kwa makufuli japo ‘mfunguaji’ alikuwa na walioifunga, kama kweli ilikuwa imefungwa? Sasa kaya ‘imefunguliwa.’ Mnataka nini kama siyo ufyatu uchwara unaowafyatua? Mnapingana na kazi ya Mungu iliyomuondoa Jiwe. Eti mwataka kitabu, sijui katibua, sijui katiba! Mshaambwa kitabu mnachotaka kibadilishwe ni makaratasi yasiyoweza kuzuia mteule kupeta hata kwa goli la mkono.

Kwa vile kimeishaumana, ishajulikana. Mafyatu weshafyatuliwa wakafyata wasifyatuke. Napendekeza tuokoe njuluku za mafyatu.

Kwa vile ‘anakubalika’ kwa kila kiumbe, mafyatu, ndege, hata wadudu kama chawa na kunguni waliotamalaki siku hizi kutokana na maajabu na miujiza, nasema kwa kinywa kipana tena kwa herufi kubwa HAKUNA MAGEUZI. No chakachuaization. Si inampendeza?

Wasusaji, chonde chonde. Msituvurugie amani kupinga visivyopingwa au kutaka kugeuza visivyogeuzwa. Mnadhani waliofyatuliwa wakapitisha hawakufanya mageuzi? Unaweza kufanya mageuzi bila mageuzi na yote ni mageuzi.

Kama mligeuzana na kupinduana, hayo hatutaki. Mnadhani mlivyochafuana na kuvuana nguo, mngekuwa na dola, si mngetekana na kupotezana? Shukuruni hamna dola.

Mafyatu tunataka mapinduzi, si mageuzi. Mapinduzi huleta amani. Mageuzi huleta machafuko. Nani anataka shari? Kawaulize wenzenu wa kaya ya jirani waliofanya mageuzi.

Kila siku, wanageuzana hadi inakera. Wamegeuzana hadi wakawageuka mafyatu. Najua wapingaji hamjakaribishwa kufyatua keki ya kaya.

Hivyo, mwawaonea maya tu. Kwa anayetaka mageuzi, anapaswa kupoka haki ndo aje na lugha ‘isiyokubalika’ ya mageuzi. Mnageuza nini wakati tulishageuzwa tangu zama za zidumu fikra za mkiti? Anayebisha aniambie. Lini tulifanya uchaguzi zaidi ya uchakachuaji na uchaguzi? Mcheke, mnune, mfyatuke, mfyate, mzoze, mzuzuke hata kuzomea, lazima mpakwa mafuta apite kama alivyoingia.

Sasa mnafyatukafyatu ili iweje? Ufyateni na kukubali kufyatuliwa au mfyatuke mfyatue tujue. Kwa nini kutaka kugeuza ‘mageuzi’ makubwa ya kidemokrasia yaliyokwishafanyika? Nani haoni haya mageuzi na maendeleo? Kama mnayaona, basi yakubalini tuendelee kutesa pasina kutesana au kuteseka na mageuzi.

Kama hamuyaoni, jifanyeni mnayaona. Kama hayapo, jifanyeni yapo, na kama hayafai, jifanye yanawafaa hata kama hayawafai. Mwataka tuwakubalie mgeuze mipango iliyopitishwa bila kupingwa? Nisisitize.

Unaweza kuchagua kwa kutochagua na kutochagua kwa kuchagua. Yote ni uchaguzi na uchaguzi ni demokrasia hata kama ghasia. Wanaotaka mageuzi, wangoje hadi Yesu arudi. Hivi leo nimekunywa ngapi?

Related Posts