Yanga yasisitiza kupeleka timu kwa Mkapa leo

WAKATI Simba ikitangaza kutocheza mechi ya leo kwa kile ilichokiita kukiukwa kwa kanuni, wenyeji wa mchezo, Yanga wamesisitiza mechi ipo palepale na wao watapeleka timu uwanjani.

Simba imefikia uamuzi huo kwa madai ya kuzuiwa kufanya mazoezi ya mwisho kama kanuni inavyoelekeza siku moja kabla ili kujiandaa na mchezo dhidi ya Yanga uliopangwa kufanyika leo, Jumamosi, Machi 08, 2025 kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam kuanzia saa 1:15 usiku.

Taarifa iliyotolewa na Yanga leo Jumamosi Machi 08, 2025, imebainisha kuwa ratiba ya mchezo huo ipo palepale na kama haitakuwa leo, hawapo tayari kucheza siku nyingine.

“Uongozi wa Young Africans SC unapenda kuutaarifu Umma kuwa mchezo wetu wa Ligi Kuu ya NBC uliopangwa kuchezwa leo tarehe 8/3/2025, dhidi ya Simba saa 1:15 usiku upo palepale na hakuna mabadiliko yoyote.

“Young Africans kama wenyeji wa mchezo tunaamini taratibu zote za mchezo kama inavyoelekezwa kwenye kanuni za Ligi Kuu ya NBC, ziko sawa na maandalizi yote yako tayari.

“Uongozi wa Young Africans SC utapeleka timu uwanja wa Benjamin Mkapa kama inavyoelekezwa kwenye kanuni na hatutakuwa tayari kucheza mchezo huu siku nyingine tofauti na leo.

“Tunawaalika uwanjani wanachama, mashabiki na wapenzi wa klabu yetu na wadau wengine waliosafiri kutoka mikoani, nchi za jirani na sehemu mbalimbali duniani kote kuja kiushuhudia mchezo huu mkubwa barani Afrika,” imeeleza taarifa hiyo iliyotolewa na Mtendaji Mkuu wa Yanga, Andre Mtine.

Wakati hayo yakiendelea, Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) imetoa tamko kwamba mechi hiyo ipo palepale kama ilivyopangwa.

Mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania, Steven Mnguto, ameiambia Mwanaspoti kuwa licha ya Simba kudai haitapeleka timu uwanjani, lakini mchezo huo upo palepale huku akiwataka mashabiki waliokata tiketi kujipanga kwenda uwanjani.

ENDELEA KUFUATILIA MWANASPOTI KWA TAARIFA ZAIDI

Related Posts