JOTO LA UCHAGUZI LAANZA KUPANDA NYARI ATAJWA

Na Mwandishi wetu, Mirerani
JOTO la uchaguzi limeanza kupanda kwenye baadhi ya majimbo katika mchakato wa ubunge na udiwani nchini kwani baadhi wameanza kutajwa tajwa sehemu tofauti.
Ikiwa kipenga cha mchakato huo bado hakijapulizwa rasmi ila maeneo mbalimbali majina tofauti yameanza kutajwatajwa.
Miongoni mwa wadau wa maendeleo wanaotajwa tajwa kuwania ubunge mwaka 2025 ni mfanyabiashara wa jijini la Arusha na mji mdogo wa Mirerani, Justin Nyari.
Nyari ambae kisiasa amekulia ndani ya CCM na ambae amewahi kushika nafasi mbalimbali ikiwemo Kamanda wa UVCCM Wilaya ya Simanjiro, Diwani wa Kata ya Mirerani mwaka 2010/2015 na mwaka 2015 aligombea ubunge jimbo la Arusha mjini kwa tiketi ya CCM na kushika nafasi ya pili.
Hata hivyo, Nyari akizungumza kwa njia ya simu na waandishi wa habari amesema ni mapema sana kuzungumza kama atagombea ubunge au hagombei kwani muda bado.
“Ni kweli nimekualia kisiasa ndani ya chama cha ccm na ninaelewa maadili, utaratibu na kanuni za chama kwani ni mapema sana kuzungumza kuwa nitagombea au sigombei ubunge,” amesema Nyari.
Amesema majimbo yanayotajwa na watu kuwa atagombea ya Simanjiro au Arusha mjini bado yanaongozwa na wabunge kupitia CCM.
“Utaratibu wa chama unajulikana wazi kuwa muda utakapofika na dirisha likiwa wazi ndiyo mchakato wa kugombea na kutangaza nia utatangazwa na viongozi wa chama,” amesema Nyari.
Nyari amesema ukifika muda wa mchakato wa uchaguzi na ukitangazwa na CCM watamuona kama atachukua fomu ya kugombea au laa.

Related Posts