Kinachofuata baada ya Mchungaji Mashimo kutupwa jela 

Dar es Salaam. Siku moja baada ya Mchungaji Daud Nkuba, maarufu Komando Mashimo, kuhukumiwa kifungo cha miaka miwili jela na kulipa fidia ya Sh5 milioni, ameamua kukata rufaa Mahakama Kuu ya Dar es Salaam kupinga huku hiyo.

Mchungaji Komando Mashimo alihukumiwa adhabu hiyo jana Jumanne, Machi 18, 2025 katika Mahakama ya Wilaya ya Kinondoni, baada ya kupatikana na hatia katika makosa mawili kwenye kesi ya jinai iliyokuwa ikimkabili mahakamani hapo.

Hukumu hiyo ilitolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Ramadhani Rugemalira, aliyesikiliza kesi hiyo, baada ya kuridhika na ushahidi wa upande wa mashitaka alidai umethibitisha mashitaka hayo bila kuacha mashaka yoyote.

Akizungumza leo Jumatano Machi 19, 2025 na Mwananchi, wakili wa Mashimo, Hekima Mwasipu amesema wameshaanza mchakato wa kukata rufaa hiyo leo katika Mahakama hiyo Kuu.

“Tayari tumeshatoa notisi ya kukata rufaa, Mahakama Kuu kutokana na kutoridhishwa na namna kesi hiyo ilivyoendeshwa,” amesema Wakili Mwasipu.

“Hapa navyozungumza na wewe (jioni) tumetoka kufuatilia leo mchana mwenendo na hukumu ili kuweza kuipitia na kujua namna gani tutakavyowasilisha katika ukataji rufaa lakini kwa bahati mbaya hatukukuta wakili kwani alikuwa katika usikilizaji wa kesi nyingine.”

Hivyo, wakili Mwasipu amesema wanatarajia kwenda tena kesho Alhamisi mahakamani hapo kufuatilia mwenendo huo na hukumu.

Katika maelezo yake amesema hawajaridhika na hukumu hiyo na ndio maana wameamua kuikatia rufaa.

Katika kesi hiyo ambayo ameeleza ilianza kusikilizwa tangu Machi 2024.

‘Alikuwa anawatetea wengine’

Mmoja wa watu wake wa karibu, Mchungaji Jacqline Chuwa amesema wamesikitishwa na mtu wao kutupwa jela kwa kosa ambalo alikuwa akiwatetea watu wengine waliokuwa wanataka kudhulumiwa ardhi yao.

“Ni masikitiko makubwa kwetu kwa kuwa kosa lililosababisha apelekwe jela alikuwa ameingilia kutetea haki za wanaoonewa, kazi ambazo amekuwa akizifanya kwa watu mbalimbali lakini kwa bahati mbaya waliomfungulia mashtaka walimgeuzia kibao na kumpa kesi hiyo,” amesema Mchungaji Jacqline na kuongeza:

“Ni kutokana na hilo, amesema ndio maana amekuwa mstari wa mbele kumsaidia kwa kuwa hata wachungaji wengine ambao wamekuwa wakipitia changamoto mbalimbali na amekuwa msaada kwao.”

Alipoulizwa ilipo familia yake, Mchungaji huyo amesema wazazi pamoja na mke wake wapo mkoani na jijini Dar es Saalam anaishi na mtoto na mdogo wake.

Mwananchi lilipomtafuta mdogo wake, hakutaka kutoa ushirikiano na kueleza yeye siyo mtu wa kuzungumza na vyombo vya habari.

Mashataka yaliyokuwa yanayomkabili

Katika kesi hiyo Komando Mashimo alikuwa anakabiliwa na mashitaka matatu yakiwamo hayo mawili; kuingia kijinai na kuharibu mali pamoja na kutishia kufanya vurugu.

Katika shitaka la kwanza, Komando Mashimo Novemba 22, 2023, maeneo ya Mbezi Luis Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam, aliingia kwa jinai katika ardhi inayomilikiwa na Frola Mwashaa.

Katika shitaka la pili katika kipindi hicho kwa makusudi na kinyume cha sheria aliharibu ujenzi wa nyumba iliyoko maeneo ya Mbezi Luis ambayo ni mali ya Frola Mwashaa.

Katika shitaka la tatu Komando Mashimo alimtishia Ramson Vicent kwa vurugu.

Katika kesi hiyo upande wa mashitaka uliwaita mashahidi watano waliotoa ushahidi mahakamani hapo na kuwasilisha vielelezo viwili, huku Komando Mashimo akijitetea yeye mwenyewe na kuita mashahidi kadhaa.

Hata hivyo, Hakimu Rugemalira katika hukumu hiyo amesema kuwa upande wa mashitaka umethibitisha mashitaka hayo mawili, yaani ya kuingia kijinai na kuharibu mali na shitaka la tatu la kutishia kufanya vurugu halikuthibitishwa.

“Baada ya kupitia ushahidi wa upande wa mashitaka na wa utetezi, Mahakama hii imeridhika kuwa upande wa mashitaka umethibitisha, shitaka la kwanza la kuingia kijinai na la pili la kuharibu mali.
“Hivyo Mahakama hii inamtia hatiani mshtakiwa katika mashitaka hayo, kama alivyoshtakiwa,” amesema Hakimu Rugemalira.

Baada ya kumtia hatiani kabla ya kusomewa adhabu, mwendesha mashitaka, Wakili wa Serikali, Rhoda Kamungu, ameieleza Mahakama upande wa mashitaka hauna kumbukumbu za nyuma za jinai za mshtakiwa, lakini akaomba mahakama itoe adhabu kali kwa mshtakiwa kama sheria inavyoelekeza.

Hata hivyo, kwa upande wake Komando Mashiko alipopewa nafasi ya kuomba shufaa (nafuu ya adhabu) ameiomba mahakama kumpunguzia adhabu akieleza ana familia inayomtegemea.

Hakimu Rugemalira baada ya kusikiliza pande zote katika hukumu hiyo amesema amezingatia maelezo ya shufaa ya mshtakiwa na upande wa mashitaka pamoja na msimamo wa sheria.
“Hivyo mshitakiwa kwa kosa la kuingia kwa jinai Mahakama inamuhukumu adhabu ya kwenda jela miezi sita, na kwa kosa la kuharibu mali mahakama hii inamuhukumu mshtakiwa adhabu ya kwenda jela miaka miwili na adhabu zote zinakwenda kwa pamoja.

“Pia utatakiwa kulipa fidia ya Sh5 milioni,” amesema Hakimu Rugemalira.
“Pia mahakama hii inakuachia huru kwa kosa la kutishia kwa vurugu kwa sababu upande wa Jamhuri umeshindwa kuthibitisha shitaka dhidi yako, hivyo utatumikia kifungo cha miaka miwili gerezani.”

Related Posts