WAFANYABIASHARA TUENDELEE KUWA NA IMANI NA RAIS SAMIA -MAJALIWA

▪️Ampongeza Kamishna TRA kwa kusimamia Weledi patika ukusanyaji wa kodi

▪️Atembelea kiwanda cha uchakataji mazao ya parachichi

WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amezitaka jumuiya za wafanyabiashara nchini kuendelea kuwa na imani na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwani amedhamiria kutatua changamoto zinazohusu masuala ya kodi.

Amesema Rais Dkt. Samia anajali changamoto za wafanyabiashara na ndio maana ameunda timu mbalimbali kwa ajili ya kufanya mapitio ya kero za wafanyabiashara wafanye kazi zao kwa uhuru.

Mheshimiwa Majaliwa ametoa kauli hiyo leo (Jumapili 23 Machi 2025) alipokuwa akijibu hoja zilizotolewa na Mwakilishi wa wafanyabiashara wa Halmashauri ya Makambako aliposimama na kuzungumza na wananchi wa eneo hilo.

“Nataka niwatoe Mashaka Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan baada ya mapendekezo yenu wafanyabiashara yale kumi na tano, kufuatia mkutano na wafanyabiashara Kariakoo ameunda tume inayofanya mapitio ya mfumo wa kodi Tanzania na inaendelea kuzunguka nchi nzima kufanya kazi hiyo.”

Aidha, amempongeza Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kusimamia vyema ukusanyaji wa mapato nchini sambamba na kuchukua hatua kwa watendaji wa Mamlaka hiyo ambao wanaenda kinyume na maadili yao ya kazi.

Pia amemtaka kamishna huyo kuendelea kuboresha programu za utoaji wa elimu kwa mlipa kodi, ili kuondoa changamoto zinazowakabili wafanya biashara kuhusu masuala ya kodi.

“Serikali hii inamtaka kila mtanzania ajue umuhimu wa kulipa kodi na tunajua kuwa sasa watanzania wengi wanajua umuhimu wa kulipa kodi.”

Katika hatua nyingine, Mheshimiwa Majaliwa ametembelea kiwanda cha uchakataji zao la parachichi cha Avo Afrika, kilichopo Mkoani Njombe.

Akizungumza na wafanyakazi na baadhi ya wananchi wanaouza bidhaa zao katika kiwanda hicho, Mheshimiwa majaliwa ametoa wito kwa wakulima wa zao la parachichi kuendelea kulima zao hilo kwani sasa zao hilo lina soko la uhakika.

“Nataka niwaambie sasa hali imebadilika parachichi ni biashara tosha, kama unataka utajiri lima parachichi, ukilima leo una uhakika wa mahali pa kuuza kwa sababu sasa wawekezaji wa uhakika wapo.”

 

Related Posts