Dar es Salaam. Wakati Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) limetangaza kuboresha miundombinu yake kwenye mikoa ya Dar es Salaam, Zanzibar na Pwani limetoa ratiba ya jinsi litakavyotekeleza kazi hiyo.
Maboresho hayo yataanza Jumamosi Februari 22 hadi 28, 2025.
Tanesco limejipanga kuboresha huduma ili kuhakikisha usambazaji wa umeme kwa wananchi unafanyika kwa ufanisi.
Kutokana na hatua hiyo, baadhi ya maeneo katika Jiji la Dar es Salaam, Zanzibar na Pwani yatakabiliwa na changamoto ya huduma ya umeme kwa siku sita mfululizo kwa nyakati tofauti kwenye baadhi ya maeneo.
Kwa mujibu wa taarifa ya Tanesco kwa vyombo vya habari ya Februari 19, 2025 hatua hiyo inalenga kutoa nafasi ya kufanyika kwa maboresho kwenye kituo cha kupokea, kupoza na kusambaza umeme cha Msongo wa Kilovoti 220 kilichopo Ubungo jijini Dar es Salaam.
Katika maboresho hayo, Tanesco litafunga mashineumba (transifoma) mpya kubwa yenye uwezo wa MVA 300 ili kukidhi mahitaji ya umeme katika maeneo husika, ikiwa ni mkakati wa kumaliza tatizo la kuzidiwa kwa mashine hiyo kutokana na ongezeko la watumiaji.