Kocha: Vijana Queens haitayumba BDL

Kocha wa timu ya Vijana Queens,    Kabiola Shomari, amesema kuondoka kwa wachezaji wake, Happy Danford na Tumaini Ndossi   kujiunga na timu ya Tausi Royals, timu yake haitatetereka.

Usajili wa timu ya Tausi Royals kwa wachezaji hao kutoka Vijana Queens, ni wa pili kwao, mwaka jana iliwasajili Diana Mwendi, Tukusubira Mwalusamba na Asumpta.

Kwa mujibu wa kocha huyo, timu ya Vijana Queens haiwezi kumzuia mchezaji yeyote kujiunga na timu  anayoipenda.

“Kikubwa zaidi timu  inayomuhitaji mchezaji, inatakiwa ifuate taratibu za uhamisho, na sisi tuweze kumruhusu,” alisema Shomari. 

Alisema baada ya kuondoka wachezaji hao, wanategemea kuwapandisha  wachezaji kutoka kikosi cha pili cha City Queens kuziba nafasi hiyo.

Hata hivyo, alisema watakaowapandisha ni wachezaji walioonyesha kiwango kizuri katika ligi ya mkoa wa Dar es Salaam (BDL) mwaka jana.

“Huu ndiyo utaratibu wetu, hatuchukui mchezaji kutoka nje, tunakuza sisi wenyewe,” alisema Shomari.

 Shomari anayefundisha pia timu ya chuo cha IFM, alisema kwa upande wa   timu Vijana ‘City Bulls’ imekuwa pia ikikuza vijana chipukizi.

Alitaja timu zilizoundwa na chipukizi hao ni Jogoo ya pili kwa  Vijana ‘City Bulls’ pamoja Yellow Jacket.

“Tunakuza wachezaji, na wachezaji wamekuwa wakichuliwa kila mwaka na timu nyingine, kama Jonas Mushi, Romaldnado waliohamia JKT  na Baraka Sabibi aliyehamia UDSM Outsiders,” alisema Shomari.

Related Posts