RAIS SAMIA ASISITIZA MASLAHI YA TAIFA KUENDELEA KUZINFATIWA KWENYE MIKATABA INAYOINGIWA

-Mikataba 1799 ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa na Hati 352 za Makubaliano zafanyiwa upekuzi – Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameitaka Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuhakikisha inaendelea kuzingatia masilahi ya nchi kwenye Mikataba mbalimbali ambayo nchi inakusudia kuingia kwakua Kikatiba Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ndiyo yenye dhamana ya Upekuzi na Tathimini ya Mikataba inayongiwa na Serikali na Taasisi zake.

Dkt. Samia ameyasema hayo wakati alipokuwa Mgeni rasmi katika Maadhimisho ya Kilele cha Siku ya Sheria Nchini yaliofanyika katika Viwanja vya Chinangali Jijini, Dodoma.

Aidha, Dkt. Samia amewataka Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuendelea kuzingatia Weledi wakati wa kufanya Upekuzi na Tathimini ya Mikataba mbalimbali ambayo Serikali inayokusudia kuingia.

“Katika kuhakikisha masilahi ya nchi yetu yanaendelea kuzingatiwa kwenye Mikataba itakayoingiwa ni lazima Watumishi wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali wawe na uwezo na ubobevu kwenye masharti ya Kimikataba yanayogusa sekta za kiuchumi na uwezo wa kusimamia mikataba hiyo”. Amesema Dkt. Samia

Kwa upande wake Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Mhe. Hamza S. Johari akizungumza wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini amesema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali imeendelea Kufanya upekuzi na tathimini kwenye Mikataba mbalimbali ambapo kwa kipindi cha kuanzia mwezi Julai hadi Desemba 2024 Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ilikuwa imepekua Mikataba 1799 na Hati za Makubaliano 352.

“Kati ya mwezi Julai hadi Disemba, 2024 jumla ya Mikataba ya Kitaifa, Kikanda na 10 Kimataifa 1,799 na Hati za Makubaliano (Memoranda of Understanding) 352 zilifanyiwa upekuzi na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.” Amesema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Katika hatua nyingine Mhe. Johari amesema kuwa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali itaendelea kuwahimiza Mawakili wa Serikali na Wanasheria wote walio katika utumishi wa umma kujiendeleza na kushiriki mafunzo ya fani mbalimbali na sio fani ya sheria tu ili waweze kufanya Upekuzi wa Mikataba na Hati za Makubaliano kwa ufanisi na ufasaha.

Nae Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Juma, awali akizungumza kabla ya kumkaribisha Mgeni rasmi, amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa mchango wake anaoutoa katika kuimarisha miundombinu ya Mahakama nchini.

“Nichukue nafasi hii kukushukuru Mhe. Rais na Serikali unayoiongoza kwa namna ambavyo umewezesha kuboreshwa kwa miundombinu mbalimbali ndani ya mahakama, tunakushuru sana kwa uwezeshaji wako mpaka sasa Mahakama tunaweza kutanua wigo wa kutoa haki kwa wananchi”. Amesema Jaji Mkuu wa Tanzania.

Vilevile Jaji Mkuu wa Tanzania amewakumbusha Watendaji mbalimbali wa Mahakama kufanya maboresho katika utendaji wao na kubadilika kifkira ili waweze kutoa huduma zenye ubora kwa wananchi.

“Kila baada ya miaka mitatu tuna kawaida ya kufanya utafiti kutumia Taasisi ya nje ili kuona kama wananchi wanaridhika na huduma zetu, na kutuwezesha kuboresha zaidi huduma tunazozitoa.” Amesema Prof. Ibrahim Juma







Related Posts