WIZARA YA AFYA SOMALIA YAICHAGUA MSD KUSHIRIKIANA KATIKA MNYORORO WA UGAVI BIDHAA ZA AFYA

 Na Mwandishi Wetu

WIZARA  ya Afya nchini Somalia imeichagua  Tanzania kupitia Bohari ya Dawa (MSD) kushirikiana kwenye masuala mbalimbali yanayohusu mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya kwa  kubadilishana uzoefu katika maeneo ya mifumo, ununuzi, usambazaji na udhibiti ubora.

Hayo yamebainishwa na watendaji wa Wizara ya Afya kutoka nchini Somalia waliotembelea Bohari ya Dawa (MSD), ambapo mwakilishi wa ugeni huo Mohamed Abdulukadiri Hersi  ameeleza kuwa  hatua mbalimbali zilizofanywa na Serikali ya  Tanzania kupitia Bohari ya Dawa katika mifumo inayotumika katika mnyororo mzima wa ugavi inayotumia tekinolojia ndio umewavutia zaidi kuja kujifunza kwa kujionea namna inavyofanya kazi na kuoana na mifumo mingine ya serikali

Hersi  ameongeza kuwa, Somalia ipo kwenye mpango wa kujenga upya mfumo wake wa ugavi wa bidhaa za afya, ikiwa ni pamoja na kuboresha utaratibu wa kufikisha bidhaa za afya kwa wananchi, hivyo kati ya nchi walizozichagua kuwa mfano ni Tanzania, ambapo kupitia MSD amesema wamemejifunza mengi ambayo watakwenda kuyatekeleza watakaporudi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa MSD Mavere Tukai, ameeleza kuwa wageni hawa wamekuja Tanzania kwa muda muafaka ambapo MSD imefanya mageuzi makubwa ya kiutendaji ikiwemo kujiendesha kibiashara, na kufanya maboresho mbalimbali katika mnyororo mzima wa ugavi wa bidhaa za afya, hivyo watajifunza mengi.


Related Posts