Josiah: Mashujaa tuko nao, Mwakyusa mzuka mwingi

WAKATI Tanzania Prisons ikiendelea kujifua kwa ajili ya mwendelezo wa Ligi Kuu Bara, Kocha Mkuu wa timu hiyo, Aman Josiah amesema kikosi chake kipo tayari na Mashujaa wajiandae kisaikolojia kuacha pointi tatu.

Prisons inatarajia kushuka uwanjani Februari 6, kuikaribisha Mashujaa kwenye Uwanja wa Sokoine, jijini Mbeya ukiwa ni wa mzunguko wa pili wa ligi hiyo na mchezo wa kwanza kwa Kocha Josiah aliyerithi mikoba ya Mbwana Makata aliyesitishiwa mkataba kutokana na matokeo mabaya na sasa kazi inamsubiri kocha huyo.

Josiah alisema wamekuwa na muda mzuri wa kujiandaa na mechi za kirafiki walizocheza kwani zimeonyesha matumaini kwake ya kufanya vizuri na kujinasua nafasi za chini.

Alisema mechi dhidi ya Mashujaa wanahitaji ushindi ili kuongeza ari, morali na nguvu kikosini akieleza kuwa maandalizi waliyofanya lazima wapinzani hao waache alama tatu Sokoine.

“Tumekuwa na maandalizi mazuri, vijana wanajituma na kuonesha nia ya ushindi, tunataka kuanza kwa kishindo mzunguko wa pili tukiwakaribisha Mashujaa, hatutaki matokeo mengine” alisema Kocha huyo.

Kipa wa timu hiyo, Edward Mwakyusa alisema mazoezi waliyonayo ikiwamo mechi za kirafiki zinawapa morali na matumaini ya kuweza kubadili matokeo waliyonayo.

“Hatupo sehemu nzuri hivyo tunapoanza mzunguko wa pili hesabu ni kutafuta pointi tatu kila mechi, naamini kila mmoja kwa uwezo na juhudi binafsi tutafikia malengo” alisema Kipa huyo.

Related Posts